Thursday 5 June 2014

Mechi tano kali zaidi kwenye Kombe la Dunia





RIO DE JANEIRO, BRAZIL
FAINALI za Kombe la Dunia zitakazochezwa Brazil zimebakiza siku chache kabla ya kuanza Alhamisi ijayo. Wakati mashabiki wa soka duniani kote wakizisubiri kwa hamu, kuna mechi tano za kukumbukwa kwenye historia ya fainali hizo zilizoanza mwaka 1930.
5. Ureno 5-3 Korea Kaskazini  - Robo fainali 1966
Benfica ilikuwa kwenye kiwango cha juu kwa klabu za Ulaya mwanzoni mwa miaka ya sitini ikiwa imeshinda mataji ya Ulaya mfululizo. Nyota wake wengi waliunda kikosi cha Ureno kwenye fainali za Kombe la Dunia za mwaka 1966. Iliwachapa mabingwa watetezi Brazil kwenye nusu fainali kabla ya kufungwa na wenyeji England. Mastaa wake wawili walikuwa kiungo Mario Coluna na straika Eusebio, ambaye alimaliza kuwa mfungaji bora kwenye fainali hizo na mabao yake tisa.
Ureno ilishinda mechi zote tatu kwenye hatua ya makundi, ikiwa imefunga mabao tisa kwa jumla na kuitupa nje Brazil. Lakini, kubwa ni vile walivyoweza kutokea nyuma kwa mabao 3-0 na kuichapa Korea Kaskazini 5-3 kwenye robo fainali, Eusebio akifunga mabao manne pekee yake.
4. Ujerumani Magharibi 3-3 Ufaransa - Nusu fainali 1982
Zikiwa zimepita siku tatu tu tangu iliposhuhudiwa mechi ya mabao matano kati ya Brazil na Italia, shughuli ilikuwa pevu kwenye nusu fainali katika fainali hizo zilizofanyika Hispania.
Ujerumani Magharibi na Ufaransa zote zilikuwa makini na zilikuwa na wachezaji mahiri akina Michel Platini, Alain Giresse, Jean Tigana, Paul Breitner, Uli Stielike na Pierre Littbarski.
Bao la mapema la Littbarski la kuongoza lilifutwa na penalti ya Platini na kufanya mechi kuwa na upinzani zaidi. Kwenye mechi hiyo kulitokea tukio la kushangaza baada ya kipa wa Ujerumani, Harald Schumacher,  kugongana na beki wa Ufaransa, Patrick Battiston na beki huyo kung’oka meno mawili. Cha ajabu mwamuzi hakupiga hata filimbi.
Mechi hiyo iliingia kwenye muda wa nyongeza na mabao mawili yalifungwa ndani ya dakika sita, Marius Tresor na Giresse na wakati ikionekana kama Ufaransa itafika fainali, lakini Ujerumani ilisawazisha kupitia Karl-Heinz Rummenigge na Klaus Fischer kabla ya mechi hiyo kufikia kwenye mikwaju ya penalti na Ujerumani ilishinda baada ya kipa Schumacher kuwagomea Didier Six na Maxime Bossis mikwaju yao kutinga kwenye wavu wake.
3. Ujerumani Magharibi 3-2 England - Robo fainali 1970
Kombe la Dunia mwaka 1970 lilishuhudia mechi nyingi za maana na tatu zikitajwa kuwa makini zaidi. Moja ya mechi hizo ni robo fainali kati ya Ujerumani Magharibi na England, ikiwa ni kama mechi ya marudiano ya fainali ya mwaka 1966.
England, iliongozwa na mastaa wake makini waliokuwa na timu hiyo tangu mwaka 1966, Bobby Moore, Bobby Charlton, Martin Peters na Geoff Hurst walicheza kwa kiwango kizuri kwenye dakika za mwanzo na kuongoza kwa mabao 2-0 yalifungwa na Alan Mullery na Peters.
Kipindi hicho Ujerumani ilikuwa timu ngumu na ilikuwa na wakali kama Franz Beckenbauer, Wolfgang Overath na Gerd Muller, kocha Helmut Schoen alimwingiza Jurgen Grabowski na kubadili kila kitu. Beckenbauer akafunga la kwanza kwa jitihada binafsi, kabla ya Uwe Seeler kufunga la pili na kufanya mechi hiyo kuingia kwenye muda wa nyongeza. Wajerumani hawakushikika tena na Muller akafunga bao la ushindi kwenye dakika 108.
2. Brazil 1-1 Ufaransa - Robo fainali 1986
Likija suala la ufundi wa ndani ya uwanja, fainali hizo za Kombe la Dunia 1986 zilikuwa kiboko zaidi. Kile kikosi matata za Ufaransa kilichotisha kwenye miaka ya themanini kikiwa na wakali kama Platini, Giresse, Tigana na Dominique Rocheteau kilikuwa kwenye zama zake za mwisho. Fainali hizo zilikuwa za mwisho pia kwa magwiji wa Brazil, Socrates, Junior na Zico.
Brazil iliiongoza kwa bao la Careca, kisha ilipoteza nafasi nyingi za kufunga kabla ya Platini kuisawazishia Ufaransa. Mashabiki wakaanza kuimba nyimbo za Zico wakitaka aingizwe, Tele Santana akafanya maamuzi na Zico akaingia uwanjani kufanya mambo yake.
Staa huyo makini alisababisha penalti, lakini kwa bahati mbaya alikosa mkwaju huo baada ya kipa Joel Bats, ambaye alikuwa mchezaji bora wa mechi kuiokoa. Ilipofika zamu ya kupita penalti, manahodha wote Socrates na Platini hawakufunga na mwisho, Ufaransa ilishinda vita.
1. Italia 4-3 Ujerumani Magharibi  - Nusu Fainali 1970
Hii ilikuwa mechi ngumu iliyofanyika Juni 17, 1970 na baada ya hapo ikatajwa kuwa ‘Mechi ya Karne’. Dakika 90 zilikuwa ngumu sana, Italia iliongoza tu katika dakika nane kupitia kwa Roberto Boninsegna aliyepiga shuti kali. Ujerumani ilicharuka kusawazisha na staa wao Beckenbauer akicheza na majeruhi yake aliisawazishia timu hiyo.
Jambo hilo lilifanya mechi hiyo kuingia kwenye muda wa nyongeza. Mabao matano yalifungwa ndani ya dakika 30 na kuifanya mechi hiyo kuwa na matokeo ya ajabu. Muller aliitanguliza Ujerumani kwa bao safi, kabla ya Tarcisio Burgnich na Gigi Riva kubadili kibao. Muller akawarudisha Ujerumani mchezoni tena kwa kusawazisha kwenye dakika 110. Lakini, mpira wa adhabu uliopigwa na Gianni Rivera uliamua matokeo ya mwisho ya mchezo huo na hatimaye Italia kuibuka uwanjani kidedea.

No comments:

Post a Comment