Friday 17 January 2014

Kocha wa Okwi, awapa dili Yanga



KOCHA wa Kagera Sugar, Jackson Mayanja raia wa Uganda, ametamka kuwa kama angekuwa na mshambuliaji Emmanuel Okwi kikosini mwake, angemtumia kama straika ili kazi yake iwe kufunga mabao tu.
Mayanja amewahi kumnoa Okwi mwaka 2012 wakati akiwa kocha msaidizi wa timu ya Taifa ya Uganda ‘The Cranes’ akisaidiana na Kocha Mkuu, Bob Williamson aliyetimuliwa na nafasi yake kuchukuliwa na Milutin Sredojevic ‘Micho’.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mayanja alisema: “Namjua Okwi ni mchezaji mzuri na atawasaidia sana Yanga mzunguko wa pili lakini kama kocha na wachezaji atakaocheza nao kwenye timu watamjulia.”
“Binafsi kwa jinsi ninavyomfahamu, Okwi ningekuwa naye kwenye timu yangu, ningemtumia kama straika wa kati na kazi yake iwe ni kufunga mabao tu,”alisema Mayanja.
Okwi alikuwa akifanya vizuri kwenye kikosi cha Simba kwani mbali na kufunga mabao pia ni mtengenezaji mzuri wa mabao ya wenzake.
Yanga imekuwa ikimtumia Okwi kama winga nafasi ambayo alikuwa akiicheza alipokuwa Simba.

No comments:

Post a Comment