Monday 20 January 2014

Marafiki wafichua siri za Ronaldo


KWA wanaomtambua tangu utoto wake, alichokifanya Jumatatu iliyopita hakikuwa kigeni kwao. Kulialia. Cristiano Ronaldo alidondosha chozi aliponyakua tuzo yake ya pili ya Mwanasoka Bora wa Dunia, lakini kitendo cha kulia na kutokwa machozi ni kitu alichokifanya sana utotoni kutokana na kukabiliwa na ugumu wa maisha.
Akiwa amezaliwa katika mji wa kimasikini sana, Madeira huko Funchal, Ureno alikuwa na sifa moja ya kulia kila mambo yake yalipokwama, lakini kwenye tukio lile la wiki iliyopita, Ronaldo alidondosha chozi la furaha baada ya kutajwa mshindi wa Ballon d’Or tuzo ambayo ilikuwa na ushindani mkubwa mbele ya Lionel Messi na Franck Ribery.
Ronaldo utotoni
Alikulia katika mji wa milima mingi kisiwani kwenye eneo lililoitwa Santo Antonio, utotoni Ronaldo alikuwa mtoto wa mama (legelege). Akiwa wa nne kwenye familia ya Dolores na Dinis, mimba ya Ronaldo ilikuwa ya bahati mbaya.
Mama yake alikuwa mpishi na baba yake alikuwa mtunza bustani wa manispaa, ambaye alikuwa ameathirika sana kwa ulevi kabla ya kufariki 2005.
Misosi ilikuwa adimu sana nyumbani kwa kina Ronaldo.
Alipozaliwa mama yake alimpa jina la Cristiano, baba yake akampa Ronaldo ikiwa ni jina la Ronald Reagan (Mwigizaji filamu na rais wa zamani wa Marekani, ambaye Dinis alikuwa kipenzi chake).
Baada ya kuandamana na baba yake kwenda kwenye klabu ya kijijini kwao, Andorinha, Ronaldo akaanza kuwa na mapenzi ya soka na kipindi hicho alikuwa akicheza na binamu yake, Nuno. Alipoanza soka, Ronaldo hakurudi tena nyuma.
Aanza kucheza beki
Francisco Afonso, mwalimu wa shula ya msingi, ambaye alikuwa kocha wa kwanza kumnoa Ronaldo, alifichua ukweli kuhusu staa huyo wa Real Madrid na timu ya taifa ya Ureno baada ya kudai mwanzoni fowadi huyo alianzia kucheza beki. “Alionekana kuwa na kitu tangu utoto wake, alikuwa na mwili mdogo sana, lakini alihitaji kufanya kitu,” anasema.
“Alianza kucheza beki kabla ya kuamua kupanda mbele kwa sababu alitaka kushiriki kila kitu. Alikuwa mahiri kwenye miguu yote na alikuwa na kasi sana kitu ambacho aliendelea kukifanyia mazoezi muda wote na kuwa bora zaidi. Soka ikawa ndiyo kila kitu kwake, asipocheza alikuwa kama mgonjwa.”
Rui Alves, rafiki kipenzi wa Ronaldo utotoni, ambaye bado wanaendeleza urafiki wao hadi sasa, anasema kitu pekee Ronaldo alichokuwa akikitaka utotoni ni kucheza soka tu.
“Tulikuwa tunakwenda kucheza siku nzima, lakini Cristiano muda wote alikuwa akipiga mpira wake,” anasema.
“Nilijaribu kumfanya acheze michezo mingine, lakini yeye alichohitaji ni soka tu. Kila jioni tulikuwa tukienda kununua mikate, lakini Ronaldo kila alipokuwa akienda lazima awe na mpira wake mkononi.” Kwenye klabu ya Andorinha, ndipo Ronaldo alipoanza  kuweka alama zake. Ricardo, aliyekuwa mchezaji mwenzake kwenye timu hiyo, ambaye kwa sasa anafanya kazi kwenye baa ya klabu hiyo, anamkumbuka Ronaldo kwa kupenda ushindani.
“Mtaani alikuwa akitaka kuwa yeye zaidi. Tangu alipokuwa mdogo, alitaka mpira muda wote uwe kwake, alipoukosa basi alichukia sana na wakati mwingine alikuwa akilia,” anasema Ricardo. Kwenye mechi moja, Cristiano aliifungia Andorinha ‘hat-trick’ (mabao matatu) kwenye kipindi cha kwanza na kuifanya timu yake kwenda mapumziko ikiwa mbele 3-0. Kipindi cha pili kilipoanza, Ronaldo aliumia kichwani na kukimbizwa hospitali kupata matibabu kabla ya kurudi uwanjani akiwa na bandeji kichwani na kuchukia zaidi kwa sababu kwa muda huo ambao yeye hakuwapo uwanjani, Andorinha ilipoteza uongozi wake wa 3-0 na kufungwa 4-3.
Kuhamia timu kubwa
Baada ya kuonyesha kuwa na kipaji, akiwa na umri wa miaka 12, hakimu wa mji wa Madeira, Joao Marques de Freitas alimpigia simu skauti wa klabu ya Sporting Lisbon, Aurelio Pereira, kujadili uwezekano wa Ronaldo kwenda kufanya majaribio kwenye klabu hiyo ya bara.
“Nilikutana na Ronaldo alikuwa na umri wa miaka 11,” anasema De Freitas. “Baba yake wa ubatizo alinitambulisha kwake na kusema ni mchezaji mzuri sana. Alikuwa mdogo sana na mwembamba sana.
“Nilichofanya niliwasiliana na mtu wa Sporting na nilimwambia: ‘Kuna mtoto hapa wanasema ni mzuri sana.’ Lakini, yeye alinijibu: ‘Huyo ni mtoto sana’ kisha akaniambia kwamba tusimpeleke mtoto mdogo kama huyo Lisbon.
“Hivyo nilizungumza na mama yake Cristiano, ambaye alikuwa mtu safi, alikubali. Hivyo tulimnunulia tiketi Ronaldo ya kwenda Lisbon na tulimfunga mfano wa kibao shingoni kilichokuwa kimeandikwa jina lake. Aurelio alikuwa stendi kumsubiri na alikaa Lisbon kwa siku nne.”
Kuna siri imefichuliwa kwamba Nacional klabu inayodai kumtengeneza Ronaldo inaidai Sporting Euro 25,000, licha ya kwamba uhamisho wake ulionekana kuwa bure. Hilo lilikuwa dau kubwa sana kwa mchezaji wa umri wa miaka 12, lakini viongozi wa klabu hizo mbili walikubaliana kufanya siri.
Atua Sporting
Hatimaye Ronaldo alitua Sporting na kujiunga na shule ya klabu hiyo inayosifika kwa kutengeneza mawingi wengi wenye viwango vya juu sana akiwamo Luis Figo.
Mama yake Ronaldo, alikuwa shabiki mkubwa sana wa Figo na pia anaishabikia Sporting, hivyo kitendo cha mwanaye kujiunga na timu hiyo kilimfanya kuwa na furaha isiyo kifani.
Mwanzoni maisha yalikuwa magumu sana kwa Ronaldo kwa sababu ya utoto wake, alikuwa akilia mara kwa mara kukumbuka nyumbani ambapo wenzake walikuwa wakimcheka sana.
Rafiki yake wa utoto, Rui anasema: “Watu hawamjui Ronaldo. Wanajifanya wanamjua, lakini ukweli ndio huo. Ronaldo ni mtu mwenye misimamo sana. Siku hizi haji Santo Antonio kwa sababu kuna watu wengi sana hawana kazi, anapokuja wanamuomba pesa tu, hivyo anaamua kukaa nao mbali. Lakini, bado hilo halimfanyi kuwa mtu mbaya.
“Bado tunawasiliana naye na baadhi ya siku tumekuwa tukifurahia maisha pamoja naye,” anasema Rui kabla ya rafiki mwingine, Ricardo kuongeza: “Inafurahisha sana, nilipokuwa mdogo nilikuwa namtazama Pauleta, aliyekuwa akitokea Azores (visiwa vingine) akichezea Ureno na nilikuwa nikiwaza kwanini na sisi kwetu Madeira kusitokee mchezaji kama wao? Kwa bahati nzuri, kwetu ametokea aliyebora zaidi.
“Ronaldo amekiweka kisiwa chetu kwenye ramani ya dunia na hakika tunashukuru kwa hilo na siku zote tutamheshimu kwa alichotufanyia.”

Kwa chozi lile alilodondosha Ronaldo mjini, Zurich haikuwa pekee tu kwake, walidondosha wengi huko Madeira kutokana na ushindi wake, eneo ambalo supastaa huyo alikua kwa umasikini mkubwa na kulialia sana kabla ya sasa kuwa mchezaji maarufu duniani.

No comments:

Post a Comment