Monday, 28 October 2013

MALINZI AANZA KAZI KWA KISHINDO,AMTOA WAMBURA KIFUNGONI

Rais mpya wa TFF, Jamal Malinzi (kulia) akiwa na rais aliyemaliza muda wake,
 Leodegar Tenga mara baada ya Malinzi kuibuka na ushindi katika uchaguzi wa shirikisho hilo
UONGOZI mpya na mambo mapya. Rais mpya wa Shirikisho  la Soka la Tanzania (TFF), Jamal Malinzi ameingia madarakani  na kasi mpya ambayo imeungwa mkono na wajumbe wa  mkutano mkuu.
Malinzi ambaye amewahi kuwa Katibu Mkuu wa Yanga,  alimshinda mshindani wake Athuman Nyamlani katika  uchaguzi mkuu wa TFF uliofanyika jijini Dar es Salaam  Jumapili iliyopita.
Uamuzi mzito alioufanya Malinzi baada ya kutangazwa Rais ni  kufuta kamati zote zilizokuwa zimeundwa na Rais aliyemaliza  muda wake, Leodegar Tenga kwa muongozo wa Fifa.
Kamati hizo ni ile ya rufaa, kamati ya rufaa ya madili, kamati  ya uchaguzi na nyinginezo ambazo zilikuwa zikitoa uamuzi wa  masuala mbalimbali ya soka la Tanzania chini ya uongozi wa  Tenga.
Malinzi pia ameshitua umma baada ya kutangaza msamaha  kwa Michael Wambura na Richard Rukambura waliokuwa  wakituhumiwa kwa makosa mbalimbali na TFF, hivyo kwa  sasa wanaruhusiwa kugombea au kuongoza soka popote. Mbali na hao, Malinzi alitangaza msamaha kwa wahanga wote  wa soka kuanzia ngazi ya wilaya mpaka Taifa ambao makosa yao hayahusiani na kutoa au kupokea rushwa.
“Tulikuwa vitani na kwenye vita kuna majeruhi, nawapa pole,  mimi pia ni miongoni mwa majeruhi wa kamati ambazo  zimekuwa zikiwahukumu watu kwa kisingizio cha maadili. 
Hata rais mpya wa nchi anapoingia madarakani anatoa  msamaha na mimi kama rais mpya wa TFF, natoa msamaha  kwa watu wote waliofungiwa kuanzia ngazi za wilaya, mikoa  mpaka Taifa,” alisema kiongozi huyo huku akishangiliwa na  wajumbe ambao baadaye aliwaongozea posho na siku moja ya  kuendelea kula bata Dar es Salaam.
“Kuna waamuzi kama akina Martin Saanya, wamefungiwa  mwaka mzima. Ila msamaha huu hauwahusu waliofungiwa  kwa masuala ya rushwa, iwe ametoa au kupokea,” alisema.
Saanya alifungiwa na Kamati ya Ligi chini ya Wallace Karia kwa kipindi cha mwaka mmoja kujihusisha na masuala ya  soka kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kuboronga katika mechi  ya mzunguko wa kwanza kati ya Yanga na Coastal.
Uamuzi wa Malinzi unarudisha matumaini ya Wambura  ambaye aliwahi kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Soka  Tanzania (FAT) kabla ya kuwa TFF, ambaye amekuwa mhanga  kwenye kamati za TFF baada ya kuenguliwa mara kwa mara  kila anapojitosa kuwania ungozi wa soka.
Wambura aliwahi kuenguliwa kwenye uchaguzi wa Simba na  baadaye uchaguzi wa Chama cha Soka cha Mara (FAM) kabla  ya kuenguliwa kwenye mchakato wa awali wa TFF akiwania  Makamu wa Rais.
Hata hivyo mchakato huo ulifutwa baada ya Fifa kuingilia kati  na kugundua dosari na kuagiza ziundwe kamati za maadili na  kamati za rufaa za maadili ambazo zingetoa hukumu kwa  Wambura na wengineo ili ijulikane wameadhibiwa kwa muda  gani.
Awali Malinzi pia alienguliwa katika mchakato wa uchaguzi  uliopangwa kufanyika Februari mwaka huu kabla ya uchaguzi  kurudiwa kwa maelekezo ya Fifa na ndipo alipoibuka na  ushindi wa kishindo.
Kwa upande wake, Wambura hakujitosa tena kuwania uongozi ndani ya shirikisho hilo kwa kile alichoeleza kuwa hawezi  kujikosha kwa maji taka.
Hata hivyo habari zinadai kwamba Wambura hakutaka kujitosa kuwania uongozi kwa hofu ya kupewa adhabu kali ambayo  pengine ingeweza kumpoteza katika medani ya soka.
Mbali na Wambura, Richard Rukambura naye ni muhanga baada ya kufungiwa miaka 30 kwa kosa la kufungua kesi  mahakamani kupinga kuenguliwa kwenye mchakato wa  uchaguzi wa awali. Pia wapo baadhi ya waamuzi ambao wamefungiwa kwa  sababu mbali mbali.
“Kwa mujibu wa katiba ya TFF, kifungo cha 44 (7) na 39 (7)
uongozi uliopita na kamati zake zote zimemaliza muda wake  tangu Desemba 13 mwaka jana, zipo kamati mpya ambazo zimeundwa juzi juzi, kuna kamati za kudumu na kamati ndogo  ndogo za kisheria kama Rais mpya naomba kibali cha mkutano mkuu kwa sababu maamuzi yote yaliyoamuliwa na mkutano  mkuu ni halali,
naombeni kibali chenu nivunje kamati zote  niunde kamati mpya,” alimalizia huku wajumbe wakijibu kwa  kishindo; “Umepata baba, sawa sawa vunja kabisa ruksa.”
Baada ya kauli hiyo Malinzi aliwafurahisha zaidi wajumbe hao  wa mkutano mkuu kwa kuwambia:
“Mlitakiwa muondoke leo  (Jumatatu) lakini mimi kama Rais mpya, naigiza sekretarieti ya  TFF iwalipe posho ya siku moja zaidi na kulala hotelini kwa  siku moja zaidi badala ya kuondoka Jumatatu mtaondoka  Jumanne (leo),”alisema Malinzi na kuzidi kushangiliwa kwa nguvu zote na wajumbe wa mkutano mkuu waliokuwa  wakipiga makofi na meza.
Wajumbe hao walilipuka zaidi kwa nderemo pale Malinzialiposema: “Viongozi wa mikoani, jiandaeni kupokea ugeni wa  kamati ya utendaji ya TFF, sasa vikao vitakuwa vinafanyika  kwa mzunguko kila mkoa na si kama ilivyozoeleka vikifanyika Dar es Salaam pekee.”

No comments:

Post a Comment